Loading...

Wabunge wataka bajeti ya barabara iongezwe


WABUNGE wameiomba serikali kuongeza bajeti ya Wakala wa Barabara Vijijini na Mijini (Tarura) kutoka asilimia 30 hadi kufikia 40 ili kuwezesha barabara nyingi za mijini na vijijini kutengenezwa.

Hata hivyo, serikali imesema inatambua kwamba kuna mahitaji makubwa ya barabara za lami nchini ambayo yanapiganiwa na wabunge, lakini Tarura itayatatua kwa awamu.

Akichangia wakati wa kuhitimisha mjadala wa Bajeti ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Naibu Waziri Tamisemi, Josephat Kandege alisema werikali inatambua kilio cha wabunge wengi cha kutaka bajeti kwa Tarura iongezeke.

Naibu wa Tamisemi, Josephat Kandege aliyasema hayo wakati wa kuhitimisha mjadala wa Bajeti ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kutokana na michango ya wabunge waliotaka bajeti ya Tarura kuongezwa kutoka asilimia 30 hadi kufikia 40.

Mbunge wa Kondoa Mjini, Edwin Sanga aliomba serikali kuangalia upya namna ya kuongeza bajeti ili itoke asilimia 30 iliyopangiwa sasa hadi kufikia asilimia 40 kutokana na Tarura unaohudumia mtandano mkubwa wa barabara. Katika bajeti ya sasa, asilimia ya 30 ya fedha zilizotengwa kwa ajili ya barabara zinakwenda Tarura wakati asilimia 70 ni zile za barabara za Tanroads.

Naibu Waziri wa Ujenzi, Elias Kwandika alisema barabara zinazounganisha mikoa ni kilomita 12,000 ambako kati ya hizo km 8,000 ni za lami na 1,700 zipo katika hatua mbalimbali za ujenzi mbazo ziko chini ya Tanroads huku barabara za mikoa na wilaya ambazo ziko chini ya Tarura ni kilomita 23,000.

Awali wakichangia Bajeti ya Wizara hiyo, Mbunge wa Rombo, Joseph Selasini (Chadema) alisema hakuna mbunge yeyote wa upinzani anayepinga utekelezaji wa miradi ya maendeleo kama ununuaji wa ndege, ujenzi wa reli.

Alisema lengo la michango yao ni kutaka serikali itekeleze miradi hiyo kwa kufuata taratibu na umakini ili fedha za wananchi zisipotee bure na kutaka ushauri wa wataalamu usikilizwe.

Mbunge wa Viti Maalumu, Munde Tambwe (CCM) aliitaka serikali kuwalipa fidia wananchi wa Mkoa wa Tabora ambao wamelazimika kuacha nyumba na maeneo yao kupisha ujenzi wa barabara mkoani humo.

Pia aliitaka serikali kuijenga kwa kiwango cha lami barabara ya Ndala-Ziba mkoani Tabora ili kurahisisha usafiri katika maeneo hayo.

Mbunge wa Ulanga Mashariki, Goodluck Mlinga (CCM) aliishukuru serikali kwa kukamilisha ujenzi wa Daraja la Kilombero kwa kiwango alichokiita cha kimataifa. Alisema daraja hilo linatarajiwa kuzinduliwa hivi karibuni na anaamini litakuwa chachu ya maendeleo ya kiuchumi jimboni kwake.

Katika mjadala huo, Mbunge wa Kilwa Kusini, Vedasto Ngombale Mwiru (CUF) aliitaka serikali kuwalipa fidia wananchi wa jimbo lake, hususan wa Kilwa Masoko ambao wamelazima kuacha maeneo yao kupisha ujenzi wa barabara.

Pia aliungana na wabunge wengine kuitaka serikali kuzifanyia ukarabati barabara za Area D mjini hapa ambazo zina hali mbaya na kuongeza kuwa uchakavu wa barabara hizo unahatarisha maisha ya viongozi na wabunge wanaoishi kwenye eneo hilo.

Mbunge wa Kinondoni, Maulid Mtulia (CCM) aliitaka Wizara hiyo kutenga bajeti kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa barabara za jimbo lake ambazo alidai nyingi zina hali mbaya.

Mbunge wa Viti Maalumu, Lucy Owenya (Chadema) aliomba serikali kutengea fedha za kuboresha uwanja wa ndege wa Moshi ambao alisema umesahaulika na kuwa kujenga kwake utasaidia kuvutia watalii na pia unaweza kusaidia wakati wa utuaji wa dharura wa ndege.

Pia ametaka reli kati ya Dar- Moshi ifufuliwe kwa haraka ambayo alisema ikikamilika itasaidia kunusuru uharibifu wa barabara unaotokana na malori ya mizigo na kuwa pia itaweza kuongeza watalii kwani kuna wengine ambao wangetaka kutumia usafiri wa treni badala ya magari na ndege.

Katika mchango wake, Owenya pia ameiomba Serikali kuuwezesha Wakala wa Ufundi na Umeme (Temesa) ili uweze kufanya kazi zake zilizokusudiwa na kuwa, kwa kufanya hivyo kutapunguza gharama kwa serikali ambapo baadhi ya magari yamekuwa yakipelekwa kwenye gereji za Wachina kwa ajili ya matengenezo.
Wabunge wataka bajeti ya barabara iongezwe Wabunge wataka bajeti ya barabara iongezwe Reviewed by Zero Degree on 4/26/2018 08:04:00 AM Rating: 5

Powered by Blogger.