Loading...

Msichana wa miaka 16 abakwa, achomwa moto India


Msichana wa miaka 16 nchini India amechomwa moto akiwa hai baada ya wazazi wake kulalamika kwa wazee wa kijiji kuwa binti huyo alibwakwa, Polisi wameeleza.

Watu 14 wamekamatwa wakihusishwa na mashambulizi hayo katika jimbo la mashariki mwa India Jharkhand.

Polisi wamesema wazee wa kijiji waliamuru wanaoshutumiwa kuhusika na ubakaji walipe faini ya rupia 50,000 sawa na pauni 550 kama adhabu.

Watu hao walighadhabishwa na maamuzi hayo na kuamua kuwapiga wazazi wa msichana huyo kisha kumchoma moto binti yao.

''Watuhumiwa wawili waliwapiga wazazi kisha wakakimbilia kwenye nyumba yao wakiwa na washirika wao na kumchoma moto msichana'' Afisa wa Polisi Ashok Ram aliliambia shirika la habari la Ufaransa.

Inaaminika kuwa msichana huyo aliachwa nyumbani wazazi wake walipokwenda harusini.

Polisi wanasema binti alibakwa na wanaume wawili katika eneo lenye msitu karibu na kijiji cha Raja Kendua.

Baada ya tukio hilo wazazi walikwenda kupeleka mashtaka kwa wazee wa kijiji kuwashtaki wabakaji.

Mabaraza ya kijiji hayana nguvu kubwa ya kisheria, hata hivyo yana ushawishi mkubwa kwenye sehemu nyingi ya vijiji vya nchini India katika kusuluhisha migogoro kuliko kutumia gharama nyingi kwenye mfumo wa mahakama.

Polisi katika jimbo hilo wamesema wamewakamata watu 14 kati ya 18 ambao watachunguzwa kutokana na madai ya ubakaji na uuaji.

mmoja kati ya watu wawili waliotajwa kufanya shambulizi hajakamatwa, alieleza Inspekta wa Polisi Shambhu Thakur alipozungumza na gazeti la Hindustan Times.

Hata hivyo, wazee kadhaa wa vijiji wamekuwa wakishutumiwa kupitisha maamuzi kinyume cha sheria na kuharibu ushahidi.

Tukio hili limekuja wakati India ikikumbwa na matukio ya uhalifu wa kingono.

Takriban matukio 40,000 ya ubakaji yameripotiwa nchini humo mwaka 2016.Matukio mengi yamekuwa hayaripotiwi kwa sababu ya unyanyapaa.

Source: BBC Swahili
Msichana wa miaka 16 abakwa, achomwa moto India Msichana wa miaka 16 abakwa, achomwa moto India Reviewed by Zero Degree on 5/05/2018 10:14:00 AM Rating: 5

Powered by Blogger.