Loading...

“Mbunge mwenye kujitambua anapaswa kutumia muda, akili na maarifa" - Kambaya


Chama cha Wananchi (CUF), kimewatuhumu wabunge wa chama hicho kwa kile ilichodai wamekuwa wakitetea na kulinda hadhi ya Katibu Mkuu wa chama hicho, Maalim Seif Sharrif Hamad kupitia Vikao vya Bunge.

Chama hicho kimedai kusikitishwa na hatua ya wabunge hao waliochaguliwa na wananchi kwa lengo la kuwakilisha matatizo yao badala yake baadhi ya yao wameacha jukumu hilo na kujipa jukumu jipya la kulinda hadhi ya Maalim Seif.

Mkurugenzi wa Habari, Uenezi na Mahusiano ya Umma wa chama hicho, Abdul Kambaya amesema ni takribani miaka miwili sasa wabunge hao kila wanaposimama hujenga hoja za kutetea Ukatibu Mkuu wa Maalim Seif badala ya kujenga zitakazotatua changamoto zilizopo kwenye majimbo yao kwa kushirikiana na serikali kupitia wizara husika.

“CUF imesikitishwa na inawaomba radhi Watanzania kutokana na vitendo vya baadhi ya wabunge hao. Ni jambo la kufedhehesha na kutia aibu sana kupokea posho na mshahara kutoka kwa walipa kodi wa Tanzania kisha unatumia miaka miwili ndani ya vikao vya Bunge kutetea hadhi ya mtu badala ya kujenga hoja zenye manufaa na walipa kodi wa Tanzania.

“Suala la Ruzuku ya CUF na Matumizi yake ni jambo la Kisheria pale ambapo CAG atabaini upotevu wa fedha hizo atatoa taarifa kwa umma, kwa hiyo kujificha kwenye hoja hiyo kwa lengo la kumfanya Maalim Seif aishi kisiasa si tu ni matumizi mabaya ya posho na mishahara inayotolewa na Bunge lakini pia ni kutotambua wajibu wao kwa wapiga kura wao waliowachagua.

“Mbunge mwenye kujitambua anapaswa kutumia muda, akili na maarifa pale apatapo fursa ya kutoa mchango wake kwa lengo la kuitaka Serikali kutatua au kushirikiana na serikali kutatua changamoto lukuki zilizopo kwenye Jimbo lake," amesema Kambaya.

Source: Mtanzania
“Mbunge mwenye kujitambua anapaswa kutumia muda, akili na maarifa" - Kambaya “Mbunge mwenye kujitambua anapaswa kutumia muda, akili na maarifa" - Kambaya Reviewed by Zero Degree on 6/06/2018 06:35:00 PM Rating: 5

Powered by Blogger.