Loading...

Hatma ya Mangula na Dk. Shein kujulikana Novemba.

KATIBU Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Abdulrahman Kinana, ametangaza nafasi za Makamu Wenyeviti wa CCM Bara, Philip Mangula na Zanzibar, Dk. Ally Mohamed Shein, zitakoma ifikapo Novemba mwaka huu.

Kinana, aliyasema hayo mjini Dodoma jana wakati wa ufunguzi wa Mkutano Mkuu maalumu ambao ulikuwa na kazi ya kupokea taarifa ya Kung’atuka kwa Mwenyekiti wa Taifa wa chama hicho, Dk. Jakaya Kikwete, pamoja na kumchagua Dk. John Magufuli kushika nafasi hiyo.

Alisema kwa mujibu wa Katiba ya CCM, Kifungu cha saba, Ibara ya 105, kifungu kidogo cha nne, Makamu Wenyeviti hao muda wao unaisha mwezi Novemba mwaka huu.

“Mkutano Mkuu Maalum wa leo, tumeandaa kwa ajili ya kumchagua Mwenyekiti wa Taifa wa CCM mpya, kwa nafasi za Makamu wenyeviti Bara na Zanzibar zinakoma mwezi Novemba,” alisema.

Katibu Mkuu huyo alipongeza Mwenyekiti mstaafu kwa hatua yake ya kukabidhi madaraka kwa hiyari na kwamba katika Katiba na kanuni ya chama hicho jambo hilo halipo, kinachofanyika ni utamaduni ulioachwa na viongozi waliopita.

Alisema lengo la viongozi waliopita kuachiana nafasi hiyo pindi anapopatikana Rais mpya ni kuweka umoja na uwajibikaji kati ya Serikali na chama.

“Dhamira hii ya Dk. Kikwete ya kutaka kung’atuka kwenye nafasi hiyo, aliitoa mwezi Februari mwaka huu mkoani Singida kwenye maadhimisho ya miaka 39 ya CCM” alisema Kinana.

Hata hivyo, aliwaambia wajumbe wa mkutano huo kuwa uliitishwa kwa mujibu wa kifungu cha saba cha Katiba ya CCM, Ibara ya 103 na kifungu kidogo cha tatu.

“Kwa mujibu wa vifungu hiki, Mkutano Mkuu maalumu wa Taifa utafanyika kwa matakwa ya Mwenyekiti wa Chama, kama ambavyo unafanyika huu na ule wa kawaida utaitishwa kama ilivyo kawaida ya taratibu za chama” alisisitiza.


Credits: IppMedia
ZeroDegree.
Hatma ya Mangula na Dk. Shein kujulikana Novemba. Hatma ya Mangula na Dk. Shein kujulikana Novemba. Reviewed by Zero Degree on 7/24/2016 10:31:00 AM Rating: 5

Powered by Blogger.