Loading...

Vigogo watano mfuko wa Maendeleo ya Jamii [ Tasaf ] wasimamishwa kazi.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Angellah Kairuki.
WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Angellah Kairuki amemuagiza Mkurugenzi Mtendaji wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (Tasaf), kuwasimamisha kazi maofisa waandamizi watano wa mfuko.

Maofisa hao ni wanaosimamia mpango huo pamoja na Meneja wa Uratibu na Mkurugenzi wa Uratibu kutokana na kushindwa kusimamia mpango wa kunusuru kaya masikini.

Kairuki alisema maofisa hao ndio viongozi wasimamizi wakuu wa mpango huo katika Awamu ya Tatu ya Tasaf na wamesimamishwa kupisha uchunguzi wa jinsi walivyohusika kuvuruga utekelezaji wa mpango huo hadi kufikia kuandikisha kaya zisizo na sifa ufanyike.
Akizungumza na waandishi wa habari jana, Dar es Salaam, Kairuki alisema ameshauriana na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi) na tayari ameshaelekeza waratibu wa Tasaf wa wilaya pia wasimamishwe kazi.

“Nimemwelekeza Mkurugenzi Mtendaji wa Tasaf awasimamishe kazi mara moja na kuendelea na hatua nyingine za kinidhamu dhidi ya maofisa washauri 106 walioko kwenye halmashauri walioshindwa kufuatilia na kusimamia mpango huu mpaka kusababisha kaya zisizostahili kuingizwa kwenye mpango na kuendelea kulipwa isivyostahili,” alisema Kairuki.

Aidha alisema ameagiza ufanyike uchunguzi wa kina kubaini ushiriki wa maofisa hao na kuchukua hatua stahiki kwa wale watakaothibitika kuhusika.

Aidha ametaka uchunguzi huo ukamilike ndani ya mwezi. Karuki alisema baada ya uhakiki kufanyika kaya 55,692 zimeondolewa kwenye mpango kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo vifo, kaya kuhama kijiji, kutojitokeza mara tatu mfululizo kupokea ruzuku, kuwa wajumbe wa kamati mbalimbali, wastaafu, viongozi na watumishi wa umma.

Alisema kuanzia Januari 2014 hadi Septemba 2016, Sh 6,427,110,309 zimeokolewa kwa kaya 42,035 zilizoondolewa kwa kipindi hicho na kwa kuwa kazi hiyo ni endelevu kuanzia Oktoba 2016 wakikamilisha kuziondoa kaya zisizostahili kiasi hicho cha fedha kinaweza kubadilika.

Hata hivyo amewaagiza Tasaf kuhakikisha wanaendelea kushirikiana na halmashauri kuongeza udhibiti wa fedha wakati wa malipo na kuhakikisha fedha zinalipwa kwa kaya zenye sifa peke yake.

Aidha, amewaagiza Tasaf kuendelea kushirikiana na halmashauri zote kukamilisha kazi ya uhakiki wa nyumba kwa nyumba katika halmashauri zote nchini kabla ya malipo yanayofuata ya Januari/ Februari 2017 kufanyika.

ZeroDegree.
Vigogo watano mfuko wa Maendeleo ya Jamii [ Tasaf ] wasimamishwa kazi. Vigogo watano mfuko wa Maendeleo ya Jamii [ Tasaf ] wasimamishwa kazi. Reviewed by Zero Degree on 12/07/2016 10:00:00 AM Rating: 5

Powered by Blogger.