Loading...

CCM matumbo moto Dodoma

MKUTANO Mkuu Maalumu wa CCM utaleta mtikisiko ndani ya chama na umefanya wajumbe kuwa matumbo moto kutokana na ajenda kubwa ya kukifanyia mageuzi, kwa kubadilisha Katiba yake na kupunguza wajumbe wa mikutano ya chama.

Mtikisiko uliopo unatokana na chama hicho, kuitisha mkutano huo kubadilisha Katiba yake ya mwaka 1977 ambayo ilifanyiwa marekebisho yake kwa mara ya mwisho mwaka 2012. Haijafanyiwa marekebisho mengine kwa zaidi ya miaka mitano.

Matumbo moto ya wajumbe yanatokana na azma ya mkutano huo, utakaofanyika katika ukumbi wa Dodoma Conventional Centre mjini hapa, kupunguza zaidi ya nusu ya idadi ya wajumbe waliokuwa wakihudhuria mikutano ya Kamati Kuu, Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) na Mkutano Mkuu wa chama.

Mkutano Mkuu huo utakaoongozwa na Mwenyekiti wa Taifa wa CCM, Rais John Magufuli utafanyika Jumapili Machi 12, mwaka huu, ukitanguliwa na kikao cha Kamati Kuu (CC) kitakachofanyika Machi 10 na NEC itafanyika Machi 11, mwaka huu.

HabariLeo ilitembelea Makao Makuu ya Chama mjini hapa, ambapo pilika pilika za kupamba zilikuwa zikiendelea huku Chipukizi, wakiweka bendera na baadhi ya wajumbe wa vikao hiyo kutoka mikoa 31 ya Tanzania, walikuwa wakibadilisha mawazo ndani na nje ya ofisi.

Wakati upambaji ukiendelea makao makuu, pia maandalizi yalikuwa yamepamba moto katika ukumbi wa Dodoma Conventional Centre, utakapofanyikia mkutano huo, kwa kugawa na kupanga maeneo maalumu ya kukaa viongozi, wajumbe, wageni waalikwa na waandishi na hata maeneo ya maonesho ya bidhaa na huduma mbalimbali, zitakazokuwapo eneo hilo.

Taarifa iliyotolewa awali na Naibu Katibu Mkuu wa CCM-Bara, Rodrick Mpogolo, ilisema mkutano huo unafanyika kufuatia mageuzi makubwa yanayofanyika ndani ya Chama, ambayo yalihitaji kufanyika marekebisho ya kanuni na Katiba ya chama.

Katika mkutano wake na waandishi wa habari mjini hapa, Mpogolo alisema, mkutano huo una umuhimu mkubwa kutokana na ajenda ya kuangalia ratiba ya uchaguzi ndani ya chama mwaka huu, lakini hasa ya kuzifanyia marekebisho sheria mama za chama hicho kikongwe zaidi na imara barani Afrika.

Katibu wa NEC, Itikadi na Uenezi, Humphey Polepole aliahidi atazungumza kesho kuhusu mkutano huo wa kihistoria. Alidokeza kuwa ajenda kubwa ya mkutano huo ni kurekebisha sheria mama ya chama hicho.

Marekebisho yatakayofanywa na mkutano huo mkuu maalumu kuhusu Katiba ya CCM, yatafuta, kurekebisha au kuongeza kwenye marekebisho ya awali yaliyofanyika ndani ya chama tangu mwaka 1977 hadi 2012.

Katika mazungumzo, mwandishi mkongwe wa chama, Charles Charles alisema mkutano huo ni muhimu zaidi kuliko uliofanyika mwaka jana, ambao ulikuwa rasmi kwa ajili ya kupokezana kijiti cha kuongoza chama kutoka kwa mwenyekiti mstaafu, Jakaya Kikwete kwenda kwa mwenyekiti wa sasa, Rais John Magufuli.

“Pia mkutano huu ni muhimu zaidi hata kuliko wa mwaka juzi, ambao chama kilikuwa kikitafuta mgombea ndani ya chama, ambapo kulikuwa na misuguano mingi kwani kwa mara ya kwanza chama kilikuwa na wagombea zaidi ya 30 wa nafasi hiyo,” alisema.

Mchujo wa awali wa urais, ulishirikisha wagombea urais 43, ambapo wengi walienguliwa na wakabaki watano. Wengine wawili nao walienguliwa katika mchujo wa pili. Mchujo wa tatu ulishirikisha majina matatu, yaliyopigiwa kura kwenye mkutano mkuu, ambapo Rais Magufuli alishinda kwa kishindo.

Wagombea wawili kura zao hazikutosha. Charles alisema mkutano huo wa wiki hii, umeibua hamasa kubwa na kuleta matumbo moto kwa wajumbe kutokana na mkakati wa chama wa kupunguza idadi ya wajumbe wa Kamati Kuu kutoka 34 hadi 24, Halmashauri Kuu kutoka 338 hadi 234 na wajumbe wa Mkutano Mkuu kutoka 3,800 hadi takribani 1,800.

Alisema, kupunguzwa kwa idadi ya wajumbe ambao walikuwa wajumbe wa mikutano hiyo, ndiko kunaibua hofu miongoni mwao, hasa pale ambapo kwa mfano kwenye nafasi hiyo walikuwa wajumbe saba, sasa wanatakiwa kupunguzwa na kubaki mmoja.

“Kupunguza idadi ya wajumbe katika mkutano huo, kunawafanya baadhi ya wajumbe kuwa na matumbo moto kutokana na kwamba watapoteza vyeo, hasa waliokuwa wakishiriki viwili au zaidi na kwamba watabakia na cheo kimoja tu,” alisema.

Mwandishi huyo mkongwe alisema, baadhi ya wajumbe walikuwa wakitumia vyeo vingi kama kinga. Walikuwa hawajabadili kutokana na kuwa na vyeo ambavyo wanavisimamia, hivyo kuwa vigumu kuwawajibisha.

Panga hilo la chama la kupunguza wajumbe, litaenda sambamba na kufyeka idadi kubwa ya vikao katika ngazi zote za shina, tawi, kata, jimbo, wilaya, mkoa hadi taifa. Lakini, pia panga hilo litagusa jumuiya za chama za Vijana, Wanawake na Wazazi.

Mwenyekiti wa CCM, Rais Magufuli akiwa na mkewe, Mama Janeth, aliwasili mjini hapa Machi 7, mwaka huu. Mwishoni mwa mwaka jana, alisema chama hicho kimefanya mageuzi na kinalenga kupunguza wajumbe. Aliahidi angeitisha Mkutano Mkuu Maalumu ili kupunguza wajumbe na nyadhifa zao.

Mabadiliko makubwa yanayotarajiwa kufanywa CCM ni : Wajumbe wa NEC ambao sasa wapo 388, watapunguzwa hadi wajumbe 158, sawa na asilimia 40. Vikao vya kawaida vya NEC navyo sasa vitafanyika kila baada ya miezi sita, badala ya miezi minne, ilivyo sasa.

Wajumbe wa Kamati Kuu ya CCM, nao watafyekwa kutoka 34 waliopo sasa hadi 24 tu. Kwa upande wa vyeo, inapendekezwa kuwa kuanzia sasa kila mwanachama, atatakiwa kushika cheo kimoja tu; au nafasi moja tu ya uongozi wa kazi za muda wote.

Kazi hizo ni Mwenyekiti wa tawi, kijiji au mtaa, kata, jimbo, wilaya na mkoa, makatibu wa Halmashauri Kuu wa ngazi zote, Mbunge, Mwakilishi na Diwani.

Mapendekezo mengine ni kufuta vyeo ambavyo havijatamkwa kwenye Katiba ya CCM na jumuiya zake ; na mfano wa vyeo hivyo ni Mwenyekiti wa wenyeviti wa CCM, makamanda wa Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM), Washauri wa Umoja wa Wanawake (UWT) na Walezi wa Jumuiya ya Wazazi.

Source: Habari Leo
CCM matumbo moto Dodoma CCM matumbo moto Dodoma Reviewed by Zero Degree on 3/10/2017 05:27:00 PM Rating: 5

Powered by Blogger.