Loading...

CCM yafagia makatibu wa mikoa 20

CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) kimewaondoa makatibu wa mikoa 20 na wa wilaya 76 kwa lengo la kuongeza tija katika muundo na mfumo, ufanisi na kueneza itikadi yake.

Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Humphrey Polepole, alitangaza 'panga' hilo wakati akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana akieleza kuwa mageuzi makubwa yanayoendelea ndani ya chama hicho yana lengo la kuhakikisha kinakuwa cha wananchi.

"Leo (jana) chama kama ilivyo desturi yake, kimefanya uteuzi wa makatibu wa mikoa 31 nchini na makatibu wa wilaya 155 Tanzania Bara," Polepole alisema.

"Uteuzi huu unaanza mara moja leo (jana). Wote waliopata uteuzi, wanatakiwa kuripoti katika vituo vyao vya kazi mara moja.

"Kati ya makatibu wa mikoa 31, makatibu 20 ni wapya na kati ya makatibu wa wilaya 155, makatibu 76 ni wapya kabisa. Wale ambao hawajapata (rasmi taarifa za) uteuzi, wawasiliane na ofisi ya CCM ili kupata taarifa zaidi."

Polepole alisema uteuzi wa makatibu hao umezingatia maadili, weledi, jinsia na utaratibu wa kuachiana vijiti kwa kuzingatia rika.

Aliongeza kuwa CCM imefanyia kazi muundo na mfumo wake ambao sasa umeanza kuimarishwa kuanzia ngazi za mashina, matawi, kata, jimbo, wilaya, mikoa hadi taifa.

Alisema kutokana na mabadiliko ya katiba ambayo yameweka uhalali wa mageuzi, chama kimeshaonyesha mwelekeo wa aina ya viongozi wa chama ambao wanachama, umma wa Watanzania na chama kinapenda kuwa nao.

"Viongozi na watendaji hawa ni lazima na kwa mienendo yao wawe waaminifu, waadilifu, wawajibikaji, wachapakazi, wanaochukia rushwa na ubadhirifu wa mali ya umma, wanaowatanguliza watu na wanachama na siyo wao wenyewe," alisema.

Alisema CCM inaendelea kufanya mageuzi makubwa ya kiuongozi, kimuundo na kiutawala ambayo yanalenga kuongeza tija, ufanisi na kupunguza gharama za uendeshaji.

Polepole pia alitumia mkutano huo kueleza hali ya kiafya ya Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana, ambaye alisema anaendelea vizuri kwenye matibabu yake nchini India.

SOurce: Nipashe
CCM yafagia makatibu wa mikoa 20 CCM yafagia makatibu wa mikoa 20 Reviewed by Zero Degree on 3/27/2017 01:21:00 PM Rating: 5

Powered by Blogger.