Loading...

Hatimaye Miss Tanzania akabidhiwa zawadi yake

NIMEFURAHI. Mrembo wa Taifa, Diana Edward (Miss Tanzania 2016) alisema hivyo jana baada ya kukabidhiwa zawadi yake ya gari aliyostahili kupata kutokana na kushinda taji hilo katika shindano lililofanyika Oktoba mwaka jana jijini Mwanza.


Akizungumza mara baada ya kukabidhiwa zawadi hiyo, Diana aliwataka warembo wanaoshiriki katika mashindano ya Miss Tanzania kuwa wavumilivu ili kukabiliana na changamoto mbalimbali za mashindano hayo zinazotokana na matatizo ya kiuchumi.

Diana alisema kuwa uvumilivu ni suala linalotakiwa kuwapo kwa vijana na hutokea kwenye tasnia mbalimbali na kamwe isiwakatishe tamaa katika harakati za kutimiza ndoto zao.


“Nimefurahi sana kukabidhiwa gari langu, nimeisubiri kwa muda mrefu na nawakumbusha wenzangu umuhimu wa kuwa mvumilivu na kuendelea kuwa na nidhamu, na sasa kwa kupitia gari langu, nitafanya kampeni yangu ya kupiga vita mimba za utotoni na unyanyasaji kwa wanawake,” alisema Diana. 

Aliwataka warembo wengine kuendeleaa kujitokeza kushiriki katika mashindano hayo pamoja na kuona matatizo yaliyowakumba wao ni mapito.

“Mashindano haya ni mazuri sana na yanasaidia kutujenga na kutupatia kipato, tangu nimalize mashindano, nimepata 'dili' mbalimbali ambazo sikutaka kuziweka wazi kwenye jamii, zimekuwa ni shughuli zangu za kila siku,” alisema Diana. 

Mkuu wa Itifaki wa Kamati ya Miss Tanzania, Albert Makoye, aliwashukuru wadhamini kwa kufanikisha kupatikana kwa zawadi hiyo na kueleza kuwa wanaanza rasmi mchakato wa kuendesha mashindano ya mwaka huu.

Mrembo huyo amepata zawadi hiyo siku chache baada ya serikali kuitaka Kampuni ya Lino International Agency kumkabidhi kabla haijaipokonya leseni ya kuandaa shindano hilo.

Kampuni ya uzalishaji na usambazaji wa vipodozi asilia ya Grace na duka la kuuza vito (Gift Jewellers) kwa pamoja ndiyo wamenunua gari hilo aina ya Suzuki Swift yenye thamani ya Sh. milioni tisa na kukamilisha taratibu za usajili na kupewa namba T625 DKL.
Hatimaye Miss Tanzania akabidhiwa zawadi yake Hatimaye Miss Tanzania akabidhiwa zawadi yake Reviewed by Zero Degree on 5/12/2017 03:22:00 PM Rating: 5

Powered by Blogger.