Loading...

Baada ya kutimuliwa Simba SC, Omog afunguka


Aliyekuwa kocha mkuu wa timu ya Simba, Joseph Omog raia wa Cameroon amefunguka kuwa kabla ya mabosi wa timu hiyo kumtimua, alikuwa na presha kutokana na mwenendo wa timu hiyo ulivyokuwa.

Maisha ya kocha huyo Simba yalifikia tamati juzi Jumamosi baada ya mabosi wa timu hiyo kuamua kumtimua kutokana na matokeo mabaya ya klabu hiyo, hasa baada ya kutolewa kwenye Kombe la Shirikisho (FA) dhidi ya Green Warriors iliyo Daraja La Pili (SDL).

Simba ambao ni mabingwa wa kombe hilo, walitolewa kwa penalti 3-4 dhidi ya Green Warriors katika mchezo uliopigwa Uwanja wa Azam Complex, Chamazi jijini Dar, Ijumaa iliyopita.

Omog ambaye aliwahi kuifundisha Azam amesema kuwa alikuwa na presha kubwa katika klabu hiyo katika kila mchezo wao ikiwemo dhidi ya Green Warriors ambao ndio ulitamatisha maisha yake ndani ya klabu hiyo iliyo kileleni mwa ligi na pointi 23.

“Kila siku kwangu ndani ya Simba nilikuwa nina presha hasa kwenye mechi zetu bila ya kujali kwamba tulikuwa tunashinda, tunafungwa au sare, kikubwa kwangu ilikuwa ni presha kwani matokeo ya timu yalikuwa yanatazamwa na watu wengi, jambo ambalo lilikuwa linanipa hofu,” alisema Mcameroon huyo.
Baada ya kutimuliwa Simba SC, Omog afunguka Baada ya kutimuliwa Simba SC, Omog afunguka Reviewed by Zero Degree on 12/25/2017 08:03:00 PM Rating: 5

Powered by Blogger.