Loading...

Hawa hapa VIONGOZI WALIOKAA MADARAKANI muda mrefu.


Wakati Rais wa Uganda, Yoweri Museveni alipotanganza nia kutetea tena nafasi hiyo baada ya kukaa madarakani kwa miaka 30 tangu alipotwaa madaraka, uamuzi wake umeonekana kuwwashangaza wengi katika nchi hiyo na nyingine duniani.

Rais Museveni anayemaliza muhula wake wa pili, baada ya kushinda katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2011, bado anakiu ya kuendelea kuwaongoza raia wa nchi hiyo, lakini siyo wote wanaoridhia na uamuzi wake.

Kutoridhia huko kunaonekana na wengi nchini humo kuwa ni rais huyo kuzidi kutowatendea haki juu ya usawa wa kidemokrasia.

Hata nje ya Uganda, kiongozi huyo wa Chama cha National Resistance Movement (NRM), huonekana hivyo. Wapo ambao wanaona mchango wa Museveni katika kuiongoza nchi hiyo unatosha, japokuwa uamuzi bado upo mikononi mwa wananchi wenyewe kwa njia ya demokrasia ya kupiga kura.

Ni wananchi wenyewe kama wakipendezwa huenda Museveni akaendelea kuongoza Uganda kwa muhula mwingine au vinginevyo.

Lakini wakati wengi wamkitolea macho rais huyo ambaye amekaa madarakani tangu mwaka 1986, wapo pia baadhi ya marais na wakuu wa nchi mbalimbali waliokaa madarakani kwa zaidi ya miaka 30 sasa huku wengine wakikaribiana na Museveni.

Rais wa Cameroon

Ni Pauli Biya, ambaye amekuwa madarakani akiwa rais wa nchi hiyo tangu mwaka 1982. Kabla ya kuwa rais alikuwa Waziri Mkuu wa nchi hiyo tangu mwaka 1975 hadi alipochaguliwa kuwa Rais wa Cameroon.

Biya ni rais wa pili wa nchi hiyo na aliingia madarakani kupitia Chama cha People’s Democratic Movement (PDM).

Rais wa Jamuhuri ya Sahrawi

Mohamed Abdelaziz, aliingia madarakani tangu mwaka 1976 kwa tiketi ya Chama cha Polisario Front. Tangu mwaka huo hadi sasa, anatimiza miaka 40 ya kuongoza nchi hiyo.

Rais wa Guinea ya Ikweta

Huyu ni Teodoro Obiang Nguema Mbasogo. Yeye alianza kuongoza nchi hiyo tangu mwaka 1979, baada ya Rais Francisco Macias Nguema kuondolewa madarakani.

Mbasongo ambaye ni rais wa pili wa nchi hiyo, alipata nafasi hiyo kupitia chama chake cha Democratic Party. Hadi sasa ameongoza nchi hiyo kwa miaka 37.

Rais wa Angola

Jose Eduardo dos Santos ndiye rais wa nchi hiyo na ameiongoza kwa miaka 37. Dos Santos aliingia madarakani tangu mwaka 1979 kama ilivyokuwa kwa Mbasongo.

Kupitia chama chake cha Popular Movement for the Liberisation of Angola, alishinda na kuwa rais wa nchi hiyo iliyopata uhuru kutoka kwa utawala wa Wareno mwaka 1975.

Mara baada ya uhuru, Rais wa nchi hiyo alikuwa ni Agostinho Neto, ambaye kwa sasa ni marehemu.

Rais wa Zimbabwe

Ni Robert Mugabe ambaye amekuwa kiongozi mkuu wa nchi hiyo tangu mwaka 1980. Kabla ya kushika wadhifa huo alikuwa Waziri Mkuu wa nchi hiyo na kiongozi mkuu wa Serikali tangu mwaka huo Zimbabwe ilipopata uhuru. Mwaka 1989 alikuwa Rais wa Zimbabwe baada ya mabadiliko ya mfumo wa utawala.

Rais Mugabe amekuwa kiongozi wa chama cha Zimbabwe African Nationla Union – Patriotic Front (ZANU - PF). Hadi sasa rais huyo anatimiza miaka 36 ya kukaa madarakani akiongoza taifa hilo.

Kiongozi wa Iran

Huyu ni Ali Khamenei ambaye ameongoza nchi hiyo tangu mwaka 1981 hadi sasa. Tangu alipoingia madarakani hadi mwaka huu, kiongozi huyo anatimiza miaka 35 ya kuwaongoza wananchi wa taifa hilo.

Khamenei ambaye alianza kuwa rais na baadaye kupewa wadhifa wa kuwa kiongozi mkuu wa Iran ni wa pili kushika nafasi hiyo, baada ya Ruhollah Khomeini.

Waziri Mkuu wa Cambodia

Wadhifa wa Hun Sen hauna tofauti na wa Rais. Yeye ndiye kiongozi mkuu wa nchi.

Sen aliingia madarakani mwaka 1985 akawa Waziri Mkuu wa Cambodia na hadi mwaka huu ametimiza miaka 31 ya kuongoza nchi hiyo.

Rais wa Sudan

Omar Al-Bashir ndiye rais wa nchi hiyo tangu mwaka 1989 hadi sasa. Kiongozi huyo aliingia madarakani baada ya aliyekuwa Wazir Mkuu wa nchi hiyo, Sadiq al-Mahdi kuondolewa na jeshi.

Baada ya uchaguzi wa mwaka 2010, Bashir alishinda tena nafasi hiyo na kuendelea kuwa Rais wa Sudan na hadi mwaka huu, anatimiza miaka 27 ya kuwa madarakani.

Rais wa Chad

Ni Idriss Deby ambaye amekuwa Rais wa Chad tangu mwaka 1990. Hadi mwaka huu bado yupo madarakani na anatimiza miaka 26 ya kuongoza nchi hiyo.

Rais huyo ameendelea kuongoza Chad licha ya viongozi wa upinzani kupinga vikali utawala wake huku wengine wakipanga njama za kumuondoa madarakani.



Source: Mwananchi
Hawa hapa VIONGOZI WALIOKAA MADARAKANI muda mrefu. Hawa hapa VIONGOZI WALIOKAA MADARAKANI muda mrefu. Reviewed by Zero Degree on 1/14/2016 05:03:00 PM Rating: 5

Powered by Blogger.