Loading...

Kazi ya kukinasua kivuko cha MV Kilombero II ndani ya maji yakwama.


Gari la Kampuni ya Kilombero Valley Teak (KVTC) likinyanyuliwa na winchi baada kuopolewa katika Mto Kilombero mkoani Morogoro jana.


Ifakara/Kilombero. Shughuli ya kukinasua Kivuko cha MV Kilombero II ndani ya maji katika Mto Kilombero, zimekwama baada kuwapo kwa hitilafu ya umeme na kusababisha vifaa vya kunyanyua vitu vizito kushindwa kufanya kazi.

Meneja wa Wakala wa Ufundi na Umeme Tanzania (Temesa), Mhandisi Margreth Mapela alisema jana kuwa, utoaji wa kivuko hicho majini na magari mawili ulikumbwa na changamoto katika dakika za mwisho.

“Jana (juzi) hii kazi ingekuwa tayari, lakini wakati tupo katika hatua za kukiopoa kivuko, gari lilishindwa kufanya kazi kutokana na upande wa kuendesha winchi kupata hitilafu,” alisema.

Mhandisi Mapela alisema baada ya kutokea tatizo hilo, mafundi walifanya kazi ya kubaini tatizo na kugundua kifaa kimojawapo kuungua na tayari kimeagizwa kingine ili kuendelea na kazi hiyo.

Akizungumzia kuhusu kivuko cha dharura cha MV Kilombero I, Mhandisi Mapela alisema ni kibovu na hakiwezi kufanya kazi hadi kifanyiwe matengenezo.

Mhandisi Mapela alisema Kivuko cha MV Kilombero I kimeharibika rada inayosaidia kumuongoza nahodha.

Alisema baada ya kujitokeza hali hiyo, Serikali imeomba kikosi cha Jeshi la Ulinzi la Wananchi Tanzania (JWTZ) kiongeze boti nyingine ya tatu ili iweze kuvusha mizigo midogo midogo wakati wakisubiria ufumbuzi wa kudumu.

Mkuu wa Kikosi cha Uzamiaji na Uokoaji kutoka Kampuni ya M. Divers Limited Dar es Salaam, Hafidh Seif alisema wamemaliza kutoa maji katika vyumba vya maboya.

“Tumekabiliana na changamoto na tunashukuru Mungu tumezishinda kwa upande wetu, lakini isingekuwa winchi la Temesa kuharibika katika upande wa umeme bila shaka kivuko kingekuwa nchikavu,” alisema Seif.

Mkurugenzi wa kampuni hiyo, Salvatory Murungi mwenye jukumu la kutafuta gari la Benki ya CRDB inayohofiwa kuwa na mtumishi wao, Dastan Rweyumamu tawi la Ifakara, alisema kazi hiyo sasa imekuwa ngumu.

Alisema kwa siku tatu wanafanya kazi ya kutafuta gari hilo bila mafanikio.

Mmoja wa wananchi katika mji wa Ifakara, Huba Mposindawa (53) aliwaomba viongozi wa Serikali kuangalia namna ya kuwashirikisha wazee wa Ifakara na Ulanga ili kusaidia kutoa ushauri.





ZeroDegree.
Kazi ya kukinasua kivuko cha MV Kilombero II ndani ya maji yakwama. Kazi ya kukinasua kivuko cha MV Kilombero II ndani ya maji yakwama. Reviewed by Zero Degree on 2/02/2016 05:03:00 PM Rating: 5

Powered by Blogger.