Loading...

Hawa hapa makocha waliotimuliwa kinafiki

HADITHI ya Claudio Ranieri na Leicester City imeshamalizika, zimebaki stori tu. Miezi tisa baada ya kuipa Leicester taji la kwanza la Premier League kwa staili ya aina yake, Muitaliano huyo ametimuliwa kutokana na mwenendo mbovu wa klabu hiyo msimu huu.

Hakuna aliyelitegemea hili na hata Ranieri kwa upande wake hakuwaza kama angetimuliwa haraka namna hii, kwanini? Siku chache zilizopita alipokea meseji nzuri kutoka kwa uongozi wa klabu hiyo.

“Pamoja na yote yanayoendelea,” ulisema ujumbe wa klabu, Februari 7, “uongozi wa Leicester City ungependa kutoa taarifa kuwa tuko nyuma ya kocha wetu Mkuu, Claudio Ranieri na tunamsapoti kwa kila jambo.”

Nani alitarajia baada ya ujumbe huu, viongozi wa Leicester wangebadili mawazo haraka namna hii? Kauli hii ya viongozi ilimpa kujiamini na kuamini bado ana maisha marefu ndani ya klabu.

Lakini matokeo yake mambo yakawa tofauti, akatimuliwa, licha ya kupewa uhakika wa kubaki. Unafikiri yeye ni wa kwanza kufanyiwa hivi? Hapana, iko orodha ya makocha ambao walijikuta wakitimuliwa siku chache baada ya kupewa uhakika na uongozi wa klabu.

Brendan Rodgers akiwa Liverpool:



Miezi miwili baada ya kupewa uhakika, akatimuliwa Agosti 2015: Mwenyekiti wa Liverpool, Tom Werner alisema, “Kwanza kabisa, klabu ina mipango ya muda mrefu sana na tunaamini Brendan atatufikisha huko.

“Tunaamini ni mtu sahihi kwa Liverpool na ndiye atakayetuvusha kutoka hapa tulipo. Ni mtu makini kwenye suala zima la usajili na tunaamini anahitaji muda zaidi wa kuijenga klabu yetu.”

OKtoba 2015: Rodgers akatimuliwa.


Roberto Mancini akiwa Man City



Miezi miwili baada ya kupewa uhakika, akatimuliwa Machi 2013: Mkurugenzi wa Manchester City, Ferran Soriano, alisema: “Mancini ni mshindi, hakuna namna utakayoweza kukataa usiwe naye. Tunajua si rahisi kubeba taji la Premier League mara mbili mfululizo, hivyo tunamsapoti hivi sasa.”

Mei 2013: Mancini alitimuliwa.


Jose Mourinho akiwa Chelsea



Miezi miwili baada ya kupewa uhakika, akatimuliwa Oktoba 2015: Taarifa ya klabu ilitolewa kwenye mtandao ikisema: “Klabu inapenda kuweka jambo hili wazi kuwa tunamsapoti Mourinho katika kila jambo.

“Tumeongea na Jose na amesema haridhishwi na matokeo ya klabu na amepanga kuboresha kiwango cha uchezaji wetu. Tuna imani naye na tunajua ni yeye pekee atakayeturudisha kwenye ubora wetu uliozoeleka.”

Desemba 2015: Mourinho alitimuliwa.


Louis van Gaal akiwa Barcelona


Mwezi mmoja baada ya kupewa uhakika, akatimuliwa Desemba 2002: Aliyekuwa Makamu wa Rais wa Barca, Sixte Cambra, alisema: “Kocha atabaki hapa na hatuna mpango wa kufanya mabadiliko kwa sasa”.

Januari 2003: Van Gaal alitimuliwa.


Tim Sherwood akiwa Aston Villa:



Siku 10 baada ya kupewa uhakika, akatimuliwa Oktoba 2015: Mkurugenzi wa Aston Villa, Charles C Krulak alisema: “Kumtaka Tim Sherwood ashinde mechi zote zilizobaki ili aendelee kuwa hapa ni uonevu mkubwa. Mara zote tunataka kuwa na mtu kwa ajili ya mipango ya muda mrefu ya klabu.”

Oktoba 2015: Sherwood alitimuliwa.

Kenny Dalglish akiwa Liverpool



Mwezi mmoja baada ya kupewa uhakika, akatimuliwa. Aprili 2012: Mwenyekiti wa Liverpool, Tom Werner alisema: “Tuna imani kubwa na Kenny. Tuna uhakika timu itabadilika na kuwa kwenye mwenendo mzuri siku za baadaye, hatuwezi kumtupa.”

Mei 2012: Dalglish alitimuliwa


Kenny Jackett akiwa Wolves:



Siku nne baada ya kupewa uhakika, akatimuliwa. Julai 2016: Mkurugenzi wa Wolves, Jeff Shi alisema: “Najitahidi kwa uwezo wangu wote kumpa ushirikiano anaouhitaji, tuna mawazo sana na nia moja ya kupata matokeo.”

Julai 2016: Jackett alitimuliwa.


Claudio Ranieri akiwa na Leicester:


Siku 16 baada ya kupewa uhakika, akatimuliwa. Februari 2017: “Leicester tunaweka wazi kuwa tuko pamoja na kocha wetu, hatuna mpango wa kumtimua na tunashirikiana kila kitu kwa pamoja.”

Februari 2017: Ranieri alitimuliwa

Japo mwenendo wa Leicester msimu huu haukuwa vizuri, lakini ni kama viongozi wamekurupuka na kumtimua Ranieri, kocha aliyeacha rekodi kubwa kwenye historia ya klabu hiyo.
Hawa hapa makocha waliotimuliwa kinafiki Hawa hapa makocha waliotimuliwa kinafiki Reviewed by Zero Degree on 2/26/2017 05:35:00 PM Rating: 5

Powered by Blogger.